logo

MIKATABA YA UENDELEZAJI BANDARI ITAZINGATIA MASLAHI YA NCHI-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali itahakikisha kuwa mikataba ya utekelezaji wa makubaliano ya uendeshaji wa maeneo ya bandari nchini kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Dubai kupitia Kampuni ya DP World itazingatia maslahi ya nchi na kuleta manufaa kwa Taifa letu.

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatano, Juni 28, 2023) wakati akitoa hoja ya kuahirisha Mkutano wa 11 wa Bunge la 12 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambapo amesisitiza kuwa makubaliano yaliyoingiwa yanalenga kuweka msingi wa ushirikiano baina ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Dubai.

Mheshimiwa Majaliwa amesema kwa kuwa bandari ya Dar es salaam ndiyo kitovu cha huduma za bandari nchini Serikali iliamua kutafuta Kampuni yenye uwezo na uzoefu mkubwa katika uendeshaji wa bandari duniani kwa teknolojia za kisasa ili kuiwezesha bandari hiyo kufanya kazi kwa ufanisi, kuongeza mapato ya nchi na kuchagiza sekta nyingine za kiuchumi.

Amesema Serikali za Tanzania na Dubai zimeingia makubaliano kwa lengo la kuanzisha ushirikiano wa kiuchumi na wa kijamii katika uendeshaji wa maeneo ya bandari nchini kupitia Kampuni ya DP World, ambayo imeonesha kuwa na utaalamu, uwezo na uzoefu mkubwa katika uendeshaji wa bandari 190 katika nchi 68 barani Afrika, Asia, Ulaya, Amerika ya Kaskazini na Kusini.

“Kuhusu umiliki wa bandari, nilihakikishie bunge lako na wananchi kwa ujumla kwamba, kupitia Sheria ya Bandari ya Mwaka, 2004, Mamlaka ya Bandari Tanzania imekasimiwa haki ya kuwa mmiliki wa maeneo yote ya bandari nchini na haina uwezo wa kutoa umiliki huo kwa kampuni nyingine. Haki iliyopewa kwa mujibu wa sheria hiyo ni kuingia mikataba ya ushirikiano wa kupangisha na kuruhusu sekta binafsi kuendesha sehemu ya maeneo hayo.”.

#JordanMediaupdates

Frank Jordan
12345 123
Follow Us
logo

© 2023 Jordan Media. All Rights Reserved. Designed by Lylical Popcorn